Header Ads Widget

Responsive Advertisement

WATENDAJI UBORESHAJI WA DAFTARI WATAKIWA KUTEKELEZA MAJUKUMU YAO KWA UFANISI


Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mheshimiwa Balozi Omar R. Mapuri akizungumza leo tarehe 11 Agosti, 2024 wakati akifunga mafunzo ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga.

Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mheshimiwa Balozi Omar R. Mapuri amewahimiza watendaji wa uchaguzi mkoani Shinyanga kutumia elimu na ujuzi waliopata kwa ufanisi ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na sheria za uchaguzi.


Mhe. Mapuri ameyasema hayo leo tarehe 11 Agosti, 2024 wakati akifunga mafunzo ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga.

Amewaambia Maafisa hao ambao ni pamoja na Mratibu wa Uandikishaji wa Mkoa, Maafisa Waandikishaji, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ugavi, na Maafisa TEHAMA wa Halmashauri kutoka mkoa Shinyanga kuwa ni vema wakatambua uzito wa jukumu lao katika zoezi hilo la kitaifa.

Mhe. Balozi Mapuri amesisitiza umuhimu wa maafisa uboreshaji katika mkoa huo kuhakikisha kuwa wanasimamia na kuendesha zoezi la uboreshaji kwa umakini mkubwa.

Aidha, amewataka kusoma kwa makini na kuelewa maelekezo yote waliyopewa, kwani maelekezo hayo ni nyenzo muhimu za kufanikisha majukumu yao.

"Ni matarajio ya Tume kuwa, baada ya zoezi hili kukamilika, wale watakaopatiwa kadi watakuwa ni wapiga kura halali," amesisitiza Balozi Mapuri.

Amewataka maafisa hao kusimamia usambazaji wa mabango na vipeperushi mapema katika kata zote za halmashauri zao.

Balozi Mapuri pia amewataka maafisa hao kuhakikisha kuwa wanazingatia matumizi ya lugha nzuri na kuwapa kipaumbele wazee, walemavu, wajawazito, na kina mama wenye watoto wadogo katika vituo vya kuandikishia wapiga kura.

Mratibu wa Uandikishaji Mkoa wa Shinyanga, Bakari Kasinyo Mohammed amewataka kuhakikisha wanatunza vifaa vya uandikishaji ili vikaweze kutumika maeneo mengine nchini akisisitiza kuwa kutokuwa makini katika utunzaji wa vifaa hivi kutapelekea athari kubwa katika ukamilishaji wa zoezi hili muhimu.


Amesema Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura Mkoani Shinyanga utafanyika sambamba na Mkoa wa Mwanza kuanzia tarehe 21 hadi 27, Agosti, 2024 ambapo vituo vitafunguliwa saa 02:00 asubuhi na kufungwa saa 12:00 jioni.

Post a Comment

0 Comments