

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akisalimiana na Viongozi mbalimbali wakati alipowasili katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete Dodoma kushiriki Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani tarehe 05 Juni 2025.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akisikiliza maelezo kutoka kwa Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Bi. Joyce Mnunguli kuhusu Mfumo Jumuishi wa Taifa wa Usimamizi wa Mazingira (E-Mazingira) wakati akikagua mabanda ya maonesho katika Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika Kitaifa katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete Dodoma tarehe 05 Juni 2025.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akitoa maelekezo mbalimbali kwa Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira wakati akikagua mabanda ya maonesho katika Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika Kitaifa katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete Dodoma tarehe 05 Juni 2025.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akisikiliza maelezo kutoka kwa Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu kutoka Wizara ya Nishati Mhandisi Innocent Luoga kuhusu matumizi ya magari yanayotumia umeme ili kulinda mazingira wakati akikagua mabanda ya maonesho katika Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika Kitaifa katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete Dodoma tarehe 05 Juni 2025.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akishuhudia gari la usafi linalotumia umeme ili kulinda mazingira linalomilikiwa na Kampuni ya Suma JKT wakati akikagua mabanda katika Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika Kitaifa katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete Dodoma tarehe 05 Juni 2025.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akiwa na viongozi mbalimbali wakiwa katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete wakishiriki Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani tarehe
05 Juni 2025.
......................
Makamu wa
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango ametoa wito kwa kwa wadau wote wa mazingira kuendeleza mambo yote
yaliyofanyika katika maadhimisho ya mazingira ikiwa ni pamoja na upandaji miti
na uanzishwaji wa bustani za kijani.
Makamu wa Rais ametoa wito huo wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mazingira
Duniani iliyofanyika Kitaifa katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete
Mkoani Dodoma. Amewahimiza wadau hao kuhamasisha matumizi ya teknolojia za
urejelezaji wa taka ozo na za plastiki, kupunguza ukataji miti holela kwa ajili
ya kuni na mkaa na kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Aidha, Makamu wa
Rais amesema Serikali imeweka nia ya kupunguza athari za uharibifu wa mazingira
kwa kupunguza matumizi ya nishati ya kuni na mkaa kwa shughuli za kupikia.
Amesema katika kutekeleza nia hiyo, Serikali ilitoa katazo la matumizi ya kuni
na mkaa kwa taasisi zinazoandaa chakula na kulisha watu zaidi ya watu mia moja
kwa siku na kuzitaka zihamie katika matumizi ya nishati safi ya kupikia ambapo
kufikia Machi 2025 jumla ya taasisi 762 zimeanza kutumia nishati safi ya
kupikia kati ya hizo taasisi za umma ni 495 na taasisi binafsi ni 267.
Halikadhalika
Makamu wa Rais amesema jukumu la kuhamasisha na kuelimisha jamii kuhusu umuhimu
wa hifadhi ya mazingira linahitaji ushirikiano wa wadau wote katika ngazi zote.
ametoa wito kwa vyombo vya habari, taasisi zote za Serikali, binafsi na asasi
za kiraia kushirikiana katika kutoa elimu kwa jamii ili kupunguza uharibifu wa
mazingira hapa nchini kwa kiasi kikubwa.
Makamu wa Rais
amesema taarifa mbalimbali za hali ya mazingira nchini zimedhihirisha kuwepo
kwa uharibifu wa ardhi katika maeneo mbalimbali nchini, ambapo inakadiriwa kuwa
takriban asilimia 61 ya ardhi nchini iko katika hatari ya kuharibika. Amesema
uharibifu huo unachangiwa kwa kiasi kikubwa na shughuli za kibinadamu zisizo
endelevu, idadi kubwa ya mifugo isiyolingana na uwezo wa malisho, ukataji wa
misitu kwa ajili ya kuni na mkaa, uanzishaji wa mashamba mapya unaotokana na
kilimo cha kuhamahama, uchimbaji holela wa madini pamoja na upanuzi wa makazi
usiozingatia mipango miji.
Makamu wa Rais
amesema katika kukabiliana na uharibifu wa mazingira, Serikali imechukua hatua
mbalimbali za kisera na kimkakati ikiwa ni pamoja na kupitishwa kwa Sera ya
Taifa ya Mazingira ya mwaka 2021, Mpango Kabambe wa Taifa wa Hifadhi na
Usimamizi wa Mazingira (2022-2032), kuongeza kasi ya upimaji wa ardhi na
umilikishaji wa ardhi kimila.
Amesema hatua
nyingine ni pamoja na uhamasishaji wa matumizi endelevu ya ardhi hususan kilimo
mseto, kilimo cha matuta, kilimo hifadhi na mbinu endelevu za kiasili za
hifadhi ya malisho. na utekelezaji wa hatua hizi ikiwa ni pamoja na kuendelea
kuhamasisha utunzaji wa mazingira kwa ujumla.
Vilevile, Makamu
wa Rais amewahimiza wananchi kushiriki kikamilifu katika Uchaguzi Mkuu wa Rais,
Wabunge na Madiwan kwa kugombea nafasi mbalimbali za uongozi, kushiriki kampeni
ili kusikiliza sera za wagombea na kujitokeza kupiga kura siku ya uchaguzi.
Aidha amewasihi wananchi hususani vijana kudumisha hali ya utulivu na usalama
hususan katika hatua ya uteuzi wa wagombea, kampeni za uchaguzi, upigaji kura
na hata baada ya matokeo kutangazwa.
Kwa upande wake,
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Khamis Hamza Khamis amesema
kauli mbiu ya mwaka 2025 inahamasisha jamii kupunguza matumizi ya bidhaa za
plastiki kwa kuwa na uzalishaji na ulaji endelevu kwa lengo la kuhifadhi mito,
maziwa na bahari ili kuhifadhi mifumo ya ikolojia.
Maadhimisho ya
Siku ya Mazingira Duniani Kitaifa yamebeba kauli mbiu isemayo “Mazingira
Yetu na Tanzania Ijayo, Tuwajibike Sasa: Dhibiti Matumizi ya Plastiki”.
Imetolewa na
Ofisi ya
Makamu wa Rais
05 Juni 2025
Dodoma.